HYAC

Attack with Style, Defend with Heart

Monday 1 December 2014

ALPHONCE FELIX AWEKA REKODI SERENGETI MARATHON 2014



 Alphonce Felix



Wanariadha Catherine Lange, Alphonce Felix na Johnson Jabir wameng’ara katika mbio za Serengeti Marathon 2014 zilizofanyika mwishoni mwa juma mkoani Simiyu wakikimbia kilometa 21 na Rhino Fun Run 5k huku wakenya wakiwataabisha watanzania katika mbio ndefu za kilometa 42.

Catherine Lange kutoka Jeshi la Magereza mkoani Arusha aliwapita kina dada wenzake katika mbio za kilometa 21 akikimbia kwa saa 1:10.28 akifuatiwa na Failuna Abdi (saa 1:12.46) na nafasi ya tatu ikishikwa na Mary Naali aliyefukuza upepo kwa saa 1:13.10

Alphonce Felix kutoka klabu ya Riadha ya Holili Youth (HYAC) aliweka rekodi tamu ya kuvutia katika mbio hizo tangu kuanza kwake mwaka 2012 alipokimbia kwa saa 1:00.40 akifuatiwa na Michael Wambura kutoka Mwanza aliyejitupa kwa saa 1:00.58 huku Dickson Marwa akivikwa nafasi ya tatu kwa saa 1:01.05

Katika mbio za kilometa  5 mwanariadha na mwandishi habari Johnson Jabir aliweka rekodi yake ya kwanza alipofukuza upepo kwa dakika 18:25.87 akifuatiwa na mkali wa kutoka Simiyu Jeremiah Kichuli aliyekimbiza upepo kwa dakika 18:40.34 na nafasi ya tatu ikichukuliwa na Nindilo Yusto aliyekimbia kwa dakika 19:15.34

Kwa upande wa wanawake mbio za 5K Rhino Fun Run alichukua nafasi ya kwanza mwanadada kutoka England Hannah WakeField aliyekimbia kwa dakika 23:28.20 akifuatiwa na Helen Severino kutoka Tanzania aliyefukuza upepo kwa dakika 24:06.57 na nafasi ya tatu ilichukuliwa na mtanzania Masalu Lengwa aliyetumia dakika 24:07.00

Kwa upande wao raia kutoka Kenya walionekana imara sana katika mbio za kilometa 42 walipowatupa watanzania ambapo wanaume Abraham Too kutoka Nandi Rift Valley alitumia saa 2:07.02 ikiwa ni rekodi murua katika mbio za Serengeti Marathon tangu kuanzishwa kwake miaka mitatu iliyopita, akifuatiwa na Julius Kilimo aliyefukuza upepo kwa saa 2:07.59

Nafasi ya tatu ilichukuliwa na mkenya Duncan Kwemboi aliyekimbia kwa saa 2:08.41 akifuatiwa na mtanzania pekee aliyechomoza katika tano bora Andrew Sambu kutoka Arusha akiweka rekodi safi ya saa 2:08.51 na nafasi ya tano ilifungwa na mkenya George Nyamori aliyetumia saa 2:11.49

Hata hivyo utabe huo ulionekana kwa wanawake ambapo Beatrice Tepkoriruta aliwaburuta wanawake wenzake akitumia saa 2:40.07 akifuatiwa na Lilian Cherimo aliyekimbia kwa saa 2:40.08 na nafasi ya tatu ikichukuliwa na mkenya mwingine Dorcas Chesan aliyefukuza upepo kwa saa 2:43.40

Mtanzania pekee katika tano bora alikuwa Fabiola William kutoka Singida aliyetimua vumbi kwa saa 2:48.15 akishika nafasi ya nne huku Banuelia Brighton kutoka Moshi, Kilimanjaro akishika nafasi ya saba kwa saa 3:48.15

Klabu ya Riadha ya Holili Youth (HYAC) iliwika zaidi katika mbio za kilometa 21 huku Pascal Mombo kutoka klabuni hapo akiiwakilisha katika full marathon aliposhika nafasi ya 11 akitumia saa 2:26.58

Josephat Joshua alishika nafasi ya sita katika half marathon kutoka HYAC akikimbia kwa saa 1:02.03, Lameck Misiwa akishika nafasi ya kumi akitumia saa 1:02.55 na Deo Hazard akitumia saa 1:03.17 na kushika nafasi ya 11.

Kwa upande wa wanawake kutoka HYAC, Furaha Sabaya alitumia saa 1:19.44 akishika nafasi ya tano ya mbio za kilometa 21, Adelina Audax alitumia saa 1:27.32 akishika nafasi ya nane  huku Neema Mathias akishika nafasi ya 10 akifukuza upepo kwa saa 1:33.21

Mkoa wa Simiyu katika kilometa 21 ulianza kuonekana  katika nafasi ya 14, Emmanuel John alipoung’arisha mkoa huo kwa kukimbia kwa saa 1:12.33 huku mwanadada Holo Makoye akichomoza katika nafasi ya 12 alipotumia saa 1:40.48

Wakenya walioonekana katika kumi bora ya kilometa 21 ya Serengeti Marathon 2014  ni Wilson Kibrop (saa 1:01.24) akishika nafasi ya nne, Isaac Koech (saa 1:01.44) nafasi ya tano na Vincent Osoro (saa 1:02.16) aliyeshika nafasi ya saba.

Kwa upande wake mgeni wa heshima katika mbio hizo Mkuu wa Wilaya ya Bunda Joshua Mirumbe alisema Serengeti Marathon imeifanya mikoa ya Mara na Simiyu kung’ara kwa namna nyingine kimichezo kutokana na uwepo wa wanariadha kutoka mataifa mbalimbali ambayo kwa mwaka huu yaliongeza kutoka matatu mwaka uliopita hadi saba England, Scotland, Ireland, USA, Hispania, Nigeria na Kenya.

No comments:

Post a Comment