HYAC

Attack with Style, Defend with Heart

Wednesday 22 October 2014

WANARIADHA HOLILI WAPANIA ROCK CITY MARATHON OKTOBA 26




OSWALD KAHURUZI NA PASCAL MOMBO BAADA YA KUTWAA MEDALI ROTARY HALF MARATHON 2014
 


Wanariadha 9 wa Klabu ya Riadha ya Holili Youth (HYAC) wamejinasibu kufanya vizuri katika mbio zijazo za Rock City Marathon zinazotarajiwa kufanyika Oktoba 26 mwaka huu Jijini Mwanza.

Wanariadha hao walioko katika kambi ya klabu hiyo katika kijiji cha Holili kilichopo kwenye miteremko ya mlima Kilimanjaro kilometa 36 kutoka mjini Moshi ni Deo Hazard, Pascal Mombo, Elibariki Buko, Lameck Misiwa, Alphonce Felix, Josephat Joswa Neema Mathias, Adelina Audax na Lidwina Godfrey.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wanariadha hao walisema mbio hizo ni muhimu sana katika maandalizi ya mbio nyingine kubwa zijazo hapo mwakani, kwani mazoezi wamefanya ya kutosha.

“Tumefanya mazoezi ya kutosha kuelekea mbio hizo muhimu sana kwani zinatusaidia kwa maandalizi ya mbio zijazo kutokana na kuwakutanisha wakali mbalimbali wa mbio ndani na nje ya nchi.” alisema mwanariadha Deo Hazard

Kwa upande wake Kocha Timothy Kamili wa klabu hiyo alisema wanariadha wake wanakimbia katika muda mzuri kwani kuna michuano kadhaa ya hivi karibuni wamefukuza upepo kwa kiwango kinachotakiwa ni suala la marekebisho madogo ili waweze kufanya vizuri.

“Wanariadha wetu (HYAC) wanakimbia kwa kiwango cha kimataifa hivyo michuano kama hii inawaandaa zaidi katika mbio kubwa za mwakani ambazo tunaendelea kutafuta mialiko kwa ajili ya kuwapeleka ili wakaingarishe klabu na Tanzania kwa ujumla wake.”

Aidha Mkurugenzi wa Holili Youth Athletics Club, Domician Genandi alisema wanariadha wake watakimbia half marathon (kilometa 21), corporate race (kilometa 5) ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mbio zijazo ndani na nje ya nchi.

Genandi aliongeza kusema anaendelea kuwainua vijana wenye vipaji vya riadha nchini akianzia kwenye mbio fupi kuelekea mbio ndefu.

“Vipaji vya riadha vipo ni suala la uungwaji mkono kutoka kwa wadau mbalimbali, nimeanza na mbio fupi ambazo ni muhimu kwa ukuzaji wa vijana kuelekea mbio ndefu, tunaendelea kutafuta mialiko ya mbio mbalimbali nje ya nchi ili kuwapa uzoefu wanariadha wetu kwa manufaa ya taifa kwa ujumla.”

Mwanza Rock City Marathon zilizinduliwa mwezi Septemba mwaka huu na Rais wa Baraza la Michezo nchini (BMT) Dionis Malinzi ambaye aliwataka waandaji ambao ni Capital Plus International (CPI) kuendelea kuandaa mashindano hayo licha ya changamoto lukuki za riadha nchini.

Mbio hizo zitakazoanza katika Uwanja wa Kirumba na kumalizikia uwanjani humo zimedhaminiwa na taasisi mbalimbali zikiwemo NSSF, TSN Group Ltd, Bodi ya Utalii nchini  (TTB), Africa Barrick Gold, Nyanza Bottlers, Mfuko wa Pensheni (PPF), Sahara Communications, Shirika la Ndege nchini (ATCL), IPTL, TANAPA, New Mwanza Hotel na New Africa Hotel.

Rock City Marathon ilianza mwaka 2009 na kufanya kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya kukuza utalii nchini yanayofanyika kila mwishoni mwa mwaka katika Kanda ya Ziwa.

No comments:

Post a Comment